Jipatie maarifa kutoka vitabu bora vilivyoandikwa na Dr Brighton shoo kuusu imani, sayansi, afya, teknolojia, asili, malezi, saikolojia na mazingira

SHERIA YA KWANZA YA MALEZI katika ulimwengu wa kisasa

 

# 1 TENGENEZA RAMANI YA MAISHA YA MTOTO



Mtoto sio kiumbe mgeni duniani, Mtoto anapaswa kuanza kuishi katika akili za wazazi wake kabla ya kuzaliwa kwake. Kabla Binti hajaolewa anapaswa kufikiria namna anatamani mtoto wake aje kuwa, na namna atakavyomlea. Kijana wa kiume aliyetimamu anapaswa kujua mtoto wake anapaswa kuwa nani, na anapaswa kuandaa Jina la mtoto wake ambalo ndiyo maana anayohitaji mtoto wake awe.

Kwa mfano, mimi ni daktari lakini nilitamani sana kuwa mkulima, mwanangu anapaswa kuwa option ya kutimiza ndoto zangu nilizotamani kuzifanikisha ila nikafeli. Naanza kumfikiria mwanangu akiwa mkulima kujaza gepu la matamanio yangu. Watoto sio viumbe wageni, ni sehemu yetu, Mwanangu ni seli yangu. Ninapoandika vitabu, namwandikia mwanangu. ninaponunua shamba nakupanda miti ya matunda, navuta taswira binti yangu akiwa chini ya mti mzuri wa matunda. Ninapogundua kuwa Jina fulani lina sifa nzuri sana ya kufanania hali ninayotamani mwanangu aje kuipitia, naliandika katika kumbukumbu zangu litakuwa la mwanangu.

Asilimia kubwa ya watoto ambao huandaliwa njia za kupita na wazazi wao hufanikiwa. Na ndiyo maana Waigizaji wakubwa ni watoto wa watengeneza filamu wakubwa. Wanasiasa wakubwa na Marais ni  watoto wa Wanasiasa wakubwa. Wanasayansi wengi sana ni watoto wa Wanasayansi. Wafanyabiashara ni hivyohivyo. Na hata Mwana wa Mungu ni Mungu! Watoto ambao hupita njia zao na kufanikiwa sana huwa wachache sana, tena hasa wale ambao huwa na vipaji na juhudi kubwa sana, na wengi wao huwa hawarudii makosa ya kutowarithisha watoto wao.



Kama mpaka nilipokuwa na miaka 30 sikufahamu ipi ni njia bora ya kupita ya kujikimu kimaisha, kwanini nitegemee mwanangu naye aje kujitafuta mwenyewe, maana atatumia si tena miaka 30, bali hata 50. Mzazi anayezaa bila kuchora ramani ya mwanae, hana tofauti na mkulima anaemwaga mbegu zake barabarani. Ni usaliti wa hali ya juu, kama wewe umeshindwa kujipambania mwenyewe, kwanini ulete kiumbe ambaye unajua atahitaji kukutegemea, na utamkimbia.

Watu wananiuliza kwanini sitaki kujenga Nyumba yangu hapa Mjini; siwajibu. Maana sijengi kwasababu yangu, sijengi kwasababu ya mwanangu. Kijana mwenye akili timamu anapaswa kuanza kuandaa ramani ya jiografia ya mwanae ambaye yupo viunoni mwake, na ndani ya akili yake. Sijengi hapa mtaani kwasababu kuna Watu wenye maadili mabaya sana watamshawishi vibaya mwanangu. Sijengi pia kwa kuwa huu mji hakuna maji safi, maji ya Manispaa yameshamiri makemikali dawa hatari kwa afya. Mbogamboga nyingi zina madawa, siwezi kufuga hapa wanyama wangu wa asili. Sioni sehemu ambayo mwanangu atajifunza kulima bustani, au kuchunga mbuzi, Miziki wanayopiga imejaa mada za Ngono na Migogoro ya maisha, Kamwe siwezi kujenga hapa kwasababu za mwanangu.

Maisha ya Mwanadamu mpaka anapofikia hatua ya kuweza kuzalisha na kulea,  tayari ni mafanikio kwa asilimia 50%. Kuweza kumlea mwanae mpaka naye akafikia uwezo wa kuzaa, ni asilimia 100% kamili. Asili ina tabia ya kuwafanya viumbe kuzalisha au kuzaa watoto waliobora kuliko wao, na inapotokea hali za wazazi zikiwa mbaya sana, asili huwa inakataa kabisa kuzaa au kuzalisha. Na hii ndiyo sababu zama hizi kuna shida nyingi sana za uzazi, hii ni kwa kuwa; hali za maisha zimekuwa ngumu sana kiasi mifumo ya viumbe yenyewe inakataa kuzaa kutokana na kuhofia hali ngumu sana kwa watoto.

Watu wananiuliza, kwanini sitaki Kuzaa au kuzalisha! Nashindwa kuwajibu kwakuwa; siwezi si kwasababu zangu, ni kwasababu za mwanangu.  Hali yangu ya kimaisha na ya jamii yangu nilipo kwa sasa ni mbaya sana, kama mimi mwenye uzoefu mkubwa maisha yananishinda, yanini nimlete mwanangu mzuri ambaye hajui hata kujipambania.



Hili sio ombi, wala sio Ushauri, Ni jukumu la kila binadamu kuandaa Ramani ya mwanae, La sivyo Mungu, Jamii, na mwanao wote watakuhukumu kwa kuendekeza hisia za Ngono bila kujua matokeo yake kwa Kiumbe asiye na hatia.

Ni aibu kubwa sana kwa mwanaume ambaye hajui hata jina la mwanae ataitwa nani? Majina yote hata katika Biblia yalikuwa ni Maana na Matamanio ya wazazi juu ya watoto wao, hata kama hayakuwa mara nyingine kama walivyotarajia. Adamu na Eva walimwita mwanao wa kwanza Kaini, wakihisi Ni yeye atakayewaokoa na Hali waliyokuwa nayo. Ni jukumu lako pia kuhakikisha umeshaandaa kijana wako, au binti yako, anakuja kuwa nani.

Wazazi Wapumbavu!

Kama mzazi anapitia hali kama hizi chini, na bado akaamua kuzaa, anakidhi maana ya moja kwa moja ya Mpumbavu. Kosa sio hali ngumu unayopitia, kosa ni hali ngumu na bado kung’ang’ania kuzaa.

Mpaka sasa hivi maisha yangu ni magumu sana, sielewi hata njia ipi ya maisha naweza ipita ikaniletea mafanikio japo ya kujikimu binafsi. Mimi  binafsi maisha yameshanishinda natamani hata kufa. Kiukweli siwezi kulea kwa sasa hivi kutokana na haya maisha yangu, ila hata mimi mbona hakuna aliyenijali nikiwa mdogo. Watu wananichukia sana sababu ya tabia zangu mbaya, na mali zangu za wizi. Mwenza wangu ana tabia mbaya sana, hawezi acha Ulevi uliokithiri, sizani kama atakuwa na uwezo wa kujali familia yangu. Huyu mke wangu ni malaya sana, inawezekana hata mtoto wangu nikabambikizwa. Lakini Potelea mbali, Mimi nazaa tu.

Huu upumbavu ndiyo chanzo cha Mimba nyingi zinazotolewa, Watoto wengi wasio na makazi,  watoto walio katika makundi hatarishi kitabia, watoto wenye akili wanaoshindwa kuendelea na masomo, kesi nyingi za watoto yatima, na utaanza kuona hizi dalili kwa baadhi ya wazazi; utaona wakiwa hawana uzazi kwa mpango ilihali hali zao ni ngumu sana za kimaisha. Maamuzi dhaifu ya mtindo huu yatahukumiwa siku moja.

Mambo Yakuzingatia sheria ya 1

·         Unataka mtoto wako aweje kibiolojia. Angalia hali ya mwenza unayetaka kuzaa naye. Wewe ni Mfupi sana, sio mbaya ukizaa na mrefu saizi ili mwanao asiwe mfupi zaidi. Hivyo hivyo kwa mrefu sana. Ni vizuri kutengeneza ‘’Genetic diversity’’ kwa mwanao. Wazazi wasiofanana sana kijenetikia watoto wao huwa wazuri sana na wenye kinga kutokana na sababu za kijenetikia. Kuzaa na ndugu yako, au mtu mnayefanana sana kijenetikia ni hatari kama ambavyo hufanywa kwa kuku wa Broiler, ambao ni matokeo ya ‘’Selective breeding’’.

·         Unataka mtoto wako aweje kitabia. Angalia tabia ya mwenza wako, jamii atakayoishi, angalia shule atakazosoma, angalia burudani atakazoshiriki, filamu atakazoziangalia, na pia angalia vitu vya kujishughulisha ambavyo atavifanya hapo nyumbani kwako.

·         Unataka mtoto wako aweje Kiakili. Angalia Vyakula utakavyomudu kumpatia, angalia Uelewa wa mwenza wako ambaye atashiriki kumfundisha mwanao, angalia Vitabu ambavyo vipo kabatini mwako, angali kazi za kumshughulisha mwanao awe bora kiakili. Wanaume wengi wasiozingatia shida za kisaikolojia za wanawake wao ‘’Narcissistic’’ za kujipenda sana, hujikuta tayari watoto wao wakiwa Wajinga kabisa ‘’Bogus’’ kutokana na kudekezwa na mama zao. Angalia muda utakaoupata wa kuwa na mwanao, angalia pia shule, makundi ya marafiki, na walimu watakaomfundisha mwanao.

·         Unataka mwanao aweje kiafya ya mwili. Ni muhimu kujua mwanao atafanya mazoezi gani, kazi gani, na atakula vyakula gani.

·         Unataka mwanao awe kama wewe, au kama atakaokuwa nao. Ni vyema kuchagua mazingira ambayo mwanao hatakuwa na muda sana na jamii kuliko kuwa na muda na wewe.

·         Usisahau, Ni lazima mtoto kuwa chini ya uangalizi wa mzazi mmoja au wote. Kama unahisi ‘’Housegirl’’ ni mzazi, ni vema ukazaa na ‘’Housegirl’’ kuliko kuzaa na Mwanamke ambaye ana thamini kutafuta Pesa kuliko uzao wa tumbo lake. Toka wanawake walipoanza kutafuta hela haijawahi rekodiwa kuwa uchumi wa familia umeongezeka. Ni muhimu kutokuwa limbukeni wa falsafa za ujamaa, ugumu wa maisha ni matokeo ya Wabinafsi walio juu katika mifumo ya kimaisha, ila ni busara hata katika mazingira magumu; Wazazi wapambane kwa hali na mali kuwa karibu na watoto wao.

Hitimisho #1

Fumba macho yako, mwite kwa jina lake binti yako ambaye bado hajazaliwa. Mtazame alivyo mzuri na afya. Tazama mazingira aliyopo. Kumbuka, Maisha sio gharama; unahitaji chakula cha asili utakacholima au limiwa, makazi hata kama nyumba nzuri ya nyasi, mavazi rahisi hata ya ngozi, na mwisho unahitaji Upendo asilimia 100%. vingine vyote ni Tamaa na ulimbukeni.