Jipatie maarifa kutoka vitabu bora vilivyoandikwa na Dr Brighton shoo kuusu imani, sayansi, afya, teknolojia, asili, malezi, saikolojia na mazingira

SAYANSI YA HATUA KUU TATU ZA TAMAA #11

TAMAA

Sehemu hii tutaangalia hatua kuu tatu za tamaa, na maana ya tamaa. Uchambuzi umejikita sana toka kwa majaribu matatu ya Yesu. Msomaji usichanganyikiwe kwa kuanza na jaribu la kwanza, kisha la tatu, na mwisho la pili. Hatua ya pili na ya tatu ya tamaa inafanania sana, na namna nyepesi zaidi ya kuelezea ilikuwa kupitia mtindo uliotumika, lakini hoja ya msingi unaweza ipata baada ya kusoma.


HATUA KUU TATU ZA TAMAA

kama kuna jambo lenye Nguvu kubwa sana katika motisha ya kiumbe yeyote yule anayeitwa hai, basi ni tamaa. Kuna wakati hata neno tamaa hutumika kumaanisha motisha! Yaani, utendaji wowote ule wa kiumbe, huisiwa kuwa ni matokeo ya msukumo mkubwa sana wa tamaa ya huyo kiumbe juu ya jambo hilo.

Kuna mkanganyiko mkubwa sana, juu ya maana ya neno ‘’Tamaa’’ katika mantiki ya tamaa katika uasi, au tamaa katika wema. Lakini hata hivyo, tofauti ya mtu anayemtamani mke wa Jirani yake awe mkewe, na mtu anayetamani kuwa na mke kama wa Jirani yake. Imejengwa katika kiini cha tamaa kwamba, wa kwanza, anatamani kitu ‘’ambacho ni mke wa Jirani yake’’. wakati wa pili, anatamani hali ya kitu. ambacho ni ‘’tabia za nje au za ndani za mke wa Jirani yake’’.

Jambo ambalo ni baya sana kuhusu tamaa kutokana na amri ya kumi ya Mungu. kutoka kitabu cha Kutoka sura ya 20. limejengwa zaidi katika mtazamo wa kwanza, wa kutamani kitu, kuliko kutamani hali ya kitu. Hii ni kwa kuwa, hakuna vitu viwili duniani vinavyoweza kufanana katika kila kitu, kwa asilimia zote 100%. Kutamani kuwa na kitu ambacho siyo chako, lazima kutakupelekea kutaka kukichukua! Ambapo huo ndiyo mwendelezo wa maovu mengine, kama wizi, uuaji na hata uzinifu kama ubakaji.

Mtazamo wa pili wa tamaa juu ya hali ya kitu, huwa na changamoto ndogo kidogo. kwa kuwa, hali ya kitu inaweza tengenezwa bila uhitaji wa kitu husika. Na hii ni kutokana na kuwa, hali nyingi za vitu hufanana na huwa hazitegemei kitu husika. Mfano, tabia ya ucheshi, furaha, usafi, nidhamu, n.k. zinaweza letwa na kitu chochote kile. Ni kama vile namna ambavyo redio zote zinaweza tangaza taarifa ileile, hata kwa sauti ileile, lakini hakuna redio mbili duniani zilizofanana kwa asilimia 100%, hata kama zimetoka kiwanda kimoja! Kadri utakavyozichunguza kiundani zaidi, utagundua kuna utofauti, hata kama ni katika viwango vya chembechembe za atomu.

Shida ya mtazamo wa pili, imejengwa zaidi katika saikolojia ya mwenye tamaa. yaani, ni rahisi mtu kutamani mjumuisho wa tabia au hali Fulani za kitu, kwa kuhusianisha na kitu husika. mfano, mtu anatamani ucheshi, usafi, nidhamu au sifa yoyote ya mke wa Jirani yake, kama inavyotoka kwa mke wa Jirani yake moja kwa moja. Hii inadhihirisha kuwa, kiundani zaidi, huyu mtu bado ametamani kitu, namna kinavyojidhirisha. Ni sawa kabisa na mtazamo wa kwanza, ila tu hapa, haijawa kwa moja kwa moja.

TAMAA SIO MALENGO

Wengi huchanganya tamaa na malengo. lakini hii huwa ni changamoto tu ya uelewa wa maana ya tamaa. Tamaa lazima ihusishe dhamiri ya kutaka kuwa na kitu au hali ya kufanania na jambo la nje na mtu binafsi. Ili isemwe ni tamaa, lazima mtu atake kuwa na kitu anachokitaka, au hali anayoitaka, ambayo ni matokeo ya anachokiona kuwa ndicho bora zaidi. Wengi hawajui kuwa, huwezi tamani bila kuona. Lazima uone, utake, ndipo isemwe kuwa umetamani.

Ukija kwa malengo, Malengo huwa hayatoki nje. Huwa ni msukumo wa maono ya ndani. Na kama yakitokana na mtazamo wa nje, basi nayo huwa ni tamaa. Huwa napenda kusema, malengo ambayo yanahusisha sana mipango, ni matokeo ya kutazama mazingira yako, kuyatafakari, na kutengeneza taswira ya kuwa unataka kutengeneza nini. Mfano, nalenga au nafikiria kujenga saloon ya nywele maana nimeona kuna wateja wengi sana eneo hili, na ninaweza thibitisha kwa kuona hata Jirani yangu naye mwenye saloon, hushindwa kumudu idadi kubwa sana ya wateja wa nywele. Ninapovuta taswira sasa kuwa nimeshaijenga ilihali nipo katika mipango ya kuijenga, basi nakuwa nahamu ya kuikamilisha. upande wa tamaa huwa kinyume kabisa, yenyewe huanza kwa kuona saloon ya mwenzangu ikiwa na mafanikio mpaka kuzidiwa, na kisha hutoka huko kuja kwenye mipango ya mimi kufikiria hilo kama fursa kwangu.’’

Tamaa huenda kinyume na malengo, tamaa haina mipaka ya kuikamilisha, ila malengo yana mipaka. Nina mipaka ya malengo ya namna yangu ya kuoa, lakini sina mipaka ya namna yangu ya kutamani kuoa. Malengo yana kikomo kwa kuwa hutumia sana sehemu za mbele za ubongo, katika mfumo wa ubongo unaoitwa ‘’CEN’’ au ‘’central executive network’’, wakati tamaa hazina mipaka, na hutumia sana sehemu kadhaa za ndani na nyuma katika ubongo, hutumia mfumo wa ubongo unaoitwa ‘’DMN’’ au ‘’default mode network’’, mtu anayetamani anaweza zini hata akitembea, anaweza kuua ili kukamilisha au kuiba, anaweza pia akatumia njia sahihi ila bado asiwe na nia njema, kiufupi tamaa haitoki moja kwa moja sehemu za kufikiria katika Ubongo.

Changamoto: kuna watu maranyingi husema, nimemwona Mwalimu mmoja anafundisha vizuri sana, na mimi nimetamani kuwa kama yeye, Je, hiyo nayo ni tamaa mbaya?

Jibu: kwa mujibu wa Ubongo, kama umetamani namna alivyo Mwalimu, nafasi ya ualimu, au kipawa cha ualimu, namna ya kufundisha, kusaidia watu maarifa, hapo umetamani Hali. Na hilo halina shida. Na kisaikolojia hapo umetamani kwa kuwa hiyo hali ipo ndani yako, umesukumwa kuelekea asili yako. Ni kwamba umekosa neno la kutumia, umetumia tamani, badala ya kuvutiwa.

Upande wa pili kama umetamani nafasi ya Mwalimu huyo, umetamani wewe ndiyo ungekuwa katika nafasi yake, umetamani wewe ndiyo ungekuwa unasikilizwa. Wewe una dhambi ya tamaa, na inakuhatarishia afya yako ya Ubongo, na hautakuwa Mwalimu mzuri, maana huna mipaka, na hautatenda kwa upendo, utatenda kwa ubinafsi au kwa kutaka sifa.


NGUVU KUBWA YA UADUI WA TAMAA

Kabla hatujaangalia kiini cha sura hii, juu ya hatua kuu tatu za tamaa. Ni lazima tutambue kuwa, tamaa ndiye adui mkubwa zaidi wa mtu. Kama kuna kila uovu ambao mtu anaweza kuutenda kwa kutaka au kutotaka. Ambao hata yeye mwenyewe huweza kukiri kuwa hakutamani kutenda hivyo, basi sababu ya huo uovu ni tamaa. Tamaa humlazimisha mtu kutenda kwa kutaka, au kutotaka.

Katika mtazamo mpana zaidi ambao sitataka kuuzungumzia zaidi katika sehemu hii, ni kuwa, hata sayansi ya Ubongo huonyesha kuwa tamaa haina msingi katika sehemu za mbele za ubongo, au sehemu za msingi wa akili na utambuzi wa mtu. Msukumo wa tamaa ni mpana sana, kifalsafa zaidi, tamaa tutaiona kuwa imelenga parefu sana, zaidi ya malengo binafsi ya mtu. Na ndiyo maana, kama kila tamaa ya mtu ingetimia, basi tusingekuwa na Mungu mmoja leo hii duniani.

Kadri mtu anavyojifunza zaidi kuhusu tamaa, ndivyo anavyogundua zaidi kuwa, kwanini hata Suleimani alifikisha wanawake elfu wakumridhisha tu, au Nebukadneza alitaka kuabudiwa kama Mungu. Leo hii vijana hutamani umaarufu, utajiri, heshima, mamlaka, kupendwa, n.k. lakini hayo siyo malengo ya wengi wao! Unaweza gundua kuwa, wengi huwa na melengo katika fani zao, elimu zao, vipaji vyao, n.k. ajabu ni kuwa, tamaa huwa kubwa zaidi ya malengo.

tamaa huathiri hata uwezo wa malengo binafsi ya mtu. Maana, mtu hutazama malengo yake, na tamaa yake humwambia kuwa, hapo ulipo bado ni dhaifu sana. Ni kama stori ya kweli ya Lusifa, ambapo,  lengo kubwa la kipaji chake cha uimbaji bora, lilimezwa na tamaa kubwa zaidi hata ya lengo lake, tamaa ya kuwa Mungu. Naweza tamani kuwa mwalimu bora, na nikawa nikitembea katika lengo langu la kuwa mwalimu bora, lakini tamaa yaweza ua lengo hili, na kuibua hisia ya kutaka kuwa bora zaidi ya mwalimu yeyote yule anayenizunguka, au aliyewahi kuwepo. Na hapo ndipo tatizo huanza, maana hata kwa kusemwa kuwa bora zaidi ya wote, tamaa hupanda ngazi, ya kutaka kuwa sio tu mwalimu bora zaidi ya wote, bali hata kuwa bora zaidi ya wenye taaluma wote.

Unaweza thibitisha hili kwa namna ambavyo, watu walio katika ngazi bora zaidi, bado hukosa raha kwa kutoridhika na hali zao. Mfano, Malaika mkubwa zaidi Lusifa bado hakuridhika na nafasi yake, au mbunge, au Waziri Fulani, Pamoja na heshima ya nafasi yake, lakini bado hajaridhia. Na hata akiwa raisi, bado utaona hisia za kutoridhika zikiendelea kumrarua.

NAMNA TAMAA INAVYOKUUA

Unapokuwa kijana wa kiume wa miaka 7, huwezi elewa sababu ya kaka yako wa miaka 16 kutumia hela yake yote ya chakula kumnunulia zawadi mpenzi wake, na yeye kushinda njaa akitafuta tu kumridhisha mpenzi wake. Ukweli ni kuwa, alipobalehe, uhalisia wa ubongo wake ulibadilika, akapanda ngazi katika tamaa za mapenzi hatua moja zaidi ya mdogo wake. Na sasa ubongo wake una uhalisia mpya kabisa wa anavyovipenda, hii kitaalamu huitwa ‘’neuroplasticity’’.

Ndivyo pia ilivyo kwa tamaa, unapoanza ngazi za chini, unaweza usielewe kwanini kuna watu wanatamani hata waitwe Mungu, lakini kuwa makini tu usiwatukane, maana Ubongo wao umefunguka zaidi ya wa kwako, na wanaona uhalisia tofauti na uhalisia unaouona. Na wewe ukijaaliwa kukua, utaelewa wanachokiona. Sehemu hii tunaenda kuangalia ngazi kuu tatu za tamaa, huku Lusifa akiwa kielelezo cha mgonjwa mkubwa, na wa kwanza kabisa wa tamaa.

HATUA NA AINA KUU TATU ZA TAMAA

1.Uhakika Wa Kuishi na Chakula


Wengi wa watu hawajui Nguvu ya chakula namna inavyowaendesha. Tofauti na mtu kujionesha moja kwa moja kuwa ni mhanga wa uhitaji wa uhakika wa chakula, wengi huwa ni wahanga wa fedha za kujikimu za uhakika wa chakula. Popote pale mtu anaposema, ‘’ntaishije sasa!’’ mara nyingi huwa anazungumzia uhakika wa kupata chakula. kwa mavazi na makazi, asili huonekana kutokuwa na mtihani mkubwa sana, kama ilivyo kwa chakula. Idadi kubwa sana ya watu duniani, huishi katika nyumba dhaifu, nyumba za kupanga, wengine vibanda tu vya kuegesha, wengine hulala tu kwenye sehemu zenye kuwakinga, na hata wengi huwa si wakujali sana mavazi ya gharama, bali yenye kuwastili tu. Kama mtu angebakiwa na kiwango cha kukidhi hitaji moja tu kati ya matatu haya, basi angejali zaidi Chakula.

Kila anayeamka na kuendelea kupumua, ni nguvu ya chakula alichokwisha kula. Binadamu huishi kwa mkate. Inahitaji akili kubwa sana kutambua kuwa, binadamu anaweza kuishi bila mkate, na kama sivyo! Shetani asingemjaribu Yesu kwa kumwambia ‘’badili jiwe hilo kuwa mkate!’’ sayansi ya Ubongo huonesha kuwa, katika mahitaji yote ya msingi ya mwili, Ubongo huonesha kipaumbele zaidi cha motisha kwa chakula, hasa chenye kuupa mwili nishati, kama sukari. Wanasayansi wasiolijua hili, huisi labda mapenzi ndiyo huwa na kipaumbele zaidi, kama inavyoonekana kwa namna ambavyo huzalisha msisimko mkubwa sana katika ubongo, lakini hawa husahau kuwa, kama mwili usingekuwa na chakula wala mapenzi, na kuwa mhanga wa vyote mpaka mwisho, kamwe usingechagua mapenzi mbele ya chakula. Mapenzi huwa ni baada ya chakula katika ubongo. hivyo hitaji kubwa zaidi la asili katika ubongo ni chakula. Na sababu ni kuwa, binadamu huishi kwa mkate.

Msingi Wa Tamaa

Unaweza jiuliza, iwapi tamaa hapo juu. Tamaa huanzia hapa. Kwa kuwa binadamu huishi kwa chakula. Na kadri unavyoweza kuwa na uhakika wa kula, ndivyo unakuwa na uhakika wa kuishi. Binadamu hutamani sana kuwa na uhakika wa kuishi, kwa kuwa na uhakika wa chakula.

Sasa udhaifu ni kuwa, mwili huweza kula chakula kwa kiasi maalumu tu, tena chakula cha siku moja tu. Huwezi kula chakula cha leo na kesho, na kwa hivyo, kila siku kunapokucha, binadamu hupaswa kuwaza atakula nini, Au ataishi vipi kwa lugha nyingine. Swali hili huwa halipendwi kabisa na Ubongo, mtu kwa asili hutamani kuwa na uhakika wa kuishi au kula, na hivyo hitimisho pekee, huwa ni kutamani kujilimbikizia ghala. Ambapo kwa zamani za uandishi wa Injili, mfano wa Yesu humzungumzia Tajiri mpumbavu, aliyejijazia ghala, na kisha akahisi sasa, atafurahi kwa kuwa na uhakika wa kuishi. Kwasasa hivi watu hujilimbikizia mali au fedha katika mabenki, wakijitengenezea furaha kwa uhakika wa Maisha.

Unaweza jiuliza kwanini asiyemsomi au aliyemsomi, Tajiri au masikini, mwenye mamlaka au mtumwa, wote hutafuta sana Pesa. ijapokuwa hutofautiana kidogo katika matumizi, lakini wote hushea aina kuu ya utumiaji, kwa chakula. Masikini hutafuta hela ya kukidhi hitaji kuu zaidi, wakati Tajiri huongeza wigo zaidi wa mahitaji.

Maana Pana Ya Jaribu La Kwanza La Yesu

Jaribu la kwanza lilikuwa linamaanisha kuwa, kila mwanadamu hujaribiwa katika namna ambavyo ana tamaa ya kutaka uhakika wa kuishi. Mfumo wa Maisha kwa asili, huwa hautoi uhakika wa kuishi, na ndiyo maana kila mtu hupaswa kula kila siku, na siyo kula chakula cha miaka Hamsini kwa mara moja, na kuwa na uhakika wa kuishi, hata kama utatokea ukame wa chakula.

Jaribu hili ni jaribu la hatua ya kwanza ya tamaa. Yesu anafundisha kuwa, ‘’Maisha ni zaidi Chakula, na Mwili zaidi ya mavazi’’. Pia anasema ‘’Msiwaze mtakula nini au mtavaa nini’’ pia anasema ‘’Msiiwazie kesho, kesho itajiwazia yenyewe’’ na Jibu lake kwa jaribu lilikuwa ‘’Binadamu hataishi kwa mkate tu’’ Jibu hili ni la kisayansi sana, Binadamu alipoanza kuumbwa, hakuumbwa mwili na kisha akapewa chakula, na kisha akaanza kuishi, la hasha! Alipoumbwa mwili, alipuliziwa pumzi ya uhai, na kisha akaanza kuishi.

Hivyo nguvu ya kwanza kabisa ya uhai ni pumzi ya Mungu. Na baada ya Kuishi, Mungu akampatia binadamu Chakula kama chanzo endelevu cha uhai ‘’secondary source’’. Kama mtu angeufananisha mwili na Gari, basi Chakula ni kama Petroli. Katika wakati na jamii yangu kwa sasa, lita moja ya petroli inayouzwa 3,203/=Tshs,  inaweza lisukuma gari la gharama ya Milioni 250/=Tshs,  kwa umbali Fulani, kama kifanyavyo chakula kusukuma uhai wa mwili kwa siku kadhaa. italeta mantiki gani mtu mwenye gari hili kutokuwa na raha, kwa kukosa uhakika wa petroli? Au hata kulishusha kabisa thamani yake?

Lakini kama kuna ujinga mkubwa sana, ni kuamini kuwa gari linatembea kwasababu kubwa zaidi ya Petroli. Na kusahau kuwa, Ufundi uliogharimu maarifa na nishati nyingi sana, ndiyo sababu kubwa. Mpaka hapa tunaweza kugundua kuwa, Shetani hakuwa mpumbavu sana wa kutolijua hili, hata kumjaribu yesu. Ila alimjaribu kwa kuwa, alihisi naye anaweza kuwa na tamaa kama aliyonaye yeye.

Maisha Ya Tamaa Katika Hatua Ya Kwanza

Hatua hii huchukua asilimia karibia 80% kwa makadirio yangu ya rafu, ya watu wote. Asilimia kubwa sana yetu ni watu wa matabaka ya chini na kati ‘’poor & middle class’’. Na katika matabaka haya, upatikanaji wa mahitaji ya msingi kabisa, ya kuishi, ni changamoto kubwa sana. Hili huwafanya watu kuwa ni watu wa kuwaza sana, ni namna gani wanaweza kupata fedha za kukidhi mahitaji haya. Hasa pale hali inapokuwa ni ngumu, au dhiki, kama ‘’Yesu alipokuwa na njaa kwa kufunga siku 40’’. Tamaa kubwa kabisa katika hatua hii huwa, nikipata kazi! Nikipata hela! Nikivuna sana awamu hii! n.k. hisia za mtindo huu mara nyingi hujaribiwa kuhisi kuwa, kwa kukosa mahitaji hayo, basi hakuna Maisha tena.  Na hapo Shetani huwavuna wengi kama Samaki, kwa kujifanya kuwa yeye ndiye mwenye kutoa uhakika wa Maisha. kitu ambacho si kweli.

Lengo kubwa la Yesu ni kuturudisha nyuma kuwa, hakuna haja ya kutamani uhakika wa Maisha. binadamu anapaswa kujali zaidi majukumu yake, au kazi zake, na kukubaliana na kikomo cha utendaji wake, kesho ni fumbo. Kwa kuwa na lita nyingi za petroli hakumaanishi kuwa ndiyo uhakika wa kufika safari, Yesu alihitimisha mfano wake wa Tajiri mpumbavu kwa kusema, ‘’Mungu akasema leo hii naichukua nafsi yako’’. Hivyo wengi wa wanaokimbilia uhakika wa Maisha, kwa kutamani kujimbikizia mali, hujikuta tu wakiishia pabaya. Ni vema kuwa na kiasi, kuridhika na leo, na kuamini kuwa thamani ya Maisha ni kubwa kuliko chakula, kwa kuwa mwanzo wa uhai haukuwa chakula, bali neno la Bwana wetu Yesu Kristo.

2. Tamaa Ya Kutawala Asili na Ulimwengu



Akili hubadilika ghafla sana baada ya kuhisi tayari sasa nina uhakika wa kuishi kwa chakula. Binadamu huanza kutamani sasa kuwa kichwa, na kuwafanya wengine mkia. Wasomi baadhi hutafsiri vibaya sana ahadi ya Mungu ya ‘’ntakufanya kuwa kichwa na sio mkia!’’ Wao huonyesha kuwa, wanaobarikiwa huwa kichwa, au nambari moja, au viongozi,  na wasiobarikiwa huwa mkia, au wa mwisho au watumwa, Hapana, Kila mtu anaweza kuwa kichwa kama alivyo na kichwa, kutobarikiwa hulenga zaidi kutoweza kutumia kichwa, na kuwa mkia, au kutoongoza akili yako, bila shaka kuongozwa.

Yesu alipojaribiwa na Shetani kuwa, ‘’ Kama Ukinisujudia ntakupatia milki na falme zote za ulimwengu. Shetani alilenga hatua ya pili ya hisia za tamaa. Wengi huwa hawajui kwanini watu hutamani sana  kuwa wafalme, maboss, managers, machifu, viongozi, wenye ubora zaidi, nambari moja, hajawahi tokea, n.k. Falsafa ya sayansi inatusaidia sana kuelewa hili, kadri mtu anavyokuwa wa upekee sana, ndivyo thamani yake huongezeka zaidi, ndivyo watu wengi humhitaji zaidi kutokana na upekee wake, ndivyo huwa na mapokeo makubwa zaidi toka kwa watu, na ndivyo utajiri wake huongezeka zaidi. Kadri utajiri wake unavyozidi kuongezeka, ndivyo uhakika wake wa kuishi unavyoongezeka.

Kama ukimchukua kijana anayetamani kuwa Tajiri sana, na kisha ukawa ukimuuliza baadhi ya maswali kuhusu sababu ya tamaa yake, Utagundua kuwa, anatamani kuwa Tajiri sana kwa kuwa, kwa kuwa Tajiri sana atapata mengi ya mahitaji anayoyatamani, hatatumia nguvu kubwa kupata mahitaji yake au tamaa zake, atakuwa na uwezo mkubwa wa kujilinda dhidi ya hatari za Maisha.

wengi ambao huisi watu hupenda kuwa maarufu au wakubwa sana kihadhi kwa kupenda sifa toka kwa watu, huwa hawajui kuwa kupenda sifa hulenga sana uhakika wa usalama binafsi wa mtu, kimwili na kiakili. Kama atasifiwa na wengi, maana yake, uwezo wake wengi wameuona hauna wa kulinganisha naye ‘’yaani, upekee wake ni wa juu sana’’, pili wanaokusifia wanakuhakikishia kuwa wanakupenda, hivyo hawatakubali uanguke. Hizi zote zinalenga tu kumhakikishia zaidi mtu uhakika wa kuishi, kwa kujiona ya kuwa, hayuko peke yake, au yuna nguvu nyingi.

Kwa kutamani umaarufu mkubwa na mamlaka, watu wote hukutana juu. Ni kama kila mtu huongozwa kutamani sifa hizo, na hivyo, anayewahi kufika huwa na wafuasi wengi wanaotamani kuvutwa mkono. na kwakuwa kwa  umaarufu na mamlaka ni rahisi kupata marafiki wengi, wapenzi wazuri, wataalamu wakukusapoti, wasanii wa kukuburudisha. Kila aina ya kileo cha uraibu wa akili hupatikana juu. Mambo haya humfanya aliyejuu kuwa na nguvu kubwa sana, na hapa sasa ndipo kiini cha tamaa huzidi kukomaa.

Yesu alitoa somo kubwa sana ya kuwa, anayepaswa kusujudiwa ni Mungu tu, na sio mwenye nafasi yoyote ile ya juu. Alimaanisha kuwa, kwa kuwa na mamlaka na umaarufu juu ya watu, hakumaanishi kuwa thamani ya mtu huongezeka. Kwa kuwa sifa zote za Ukubwa ni za Mungu peke yake.

Uhalisia Zaidi Wa Hatua ya Pili ya Tamaa

Lusifa alishindwa kuelewa kuwa ‘’hata uwe na vitu vyote, kama huna Upendo, wewe si kitu’’. Msingi wa Ulimwengu ni Upendo, maana Mungu ni pendo. Mungu aliumba kila kitu kutoka hakuna kitu ‘’nothing’’. Biblia inaandika katika ‘’1Kor13 kuwa, hata ukiweza kusema kwa lugha za Malaika, kama huna upendo si kitu wewe. Hata ukiwa na maarifa ya kuelewa siri zote za mbinguni na duniani, kama huna upendo, si kitu wewe. Hata ukitoa mali zako zote na uwape masikini kama huna upendo, si kitu wewe. Hata ukitoa mwili wako ukachomwa moto kama huna upendo, si kitu wewe’’. Hizi zote zilikuwa ni sifa za lusifa, na ndiyo maana alimwambia hata Yesu, ntakupa kila kitu, ukinisujudia. Ajenda ya muhimu ni kuwa, Dhumuni kama sio Utukufu kwa Mungu, aliyechimbuko la Upendo, basi yote ni ubatili.

Jamii imejaa watu wenye tamaa za kuwa juu ya wengine, msingi huu wa tamaa Lusifa huujenga tangia binadamu wanapokuwa wadogo. Hii ni kupitia kuwazoeleshea ushindani katika taasisi za elimu, kupitia michezo wanayoifanya, kupitia filamu, sinema, na hata magemu wanayoyacheza. Haya yote huwachochea sana kuingia katika falsafa za kutamani kutawala wenzao, na sio tu kuwa na tamaa ya kufanikiwa. Binadamu wengi hawaridhiki kwa hali zao njema, bali huridhika kwa matokeo yao baada ya kujilinganisha na wenzao. Huu ni upumbavu mkubwa sana, haimaanishi kuwa kama umepata 30, na wanaokufuata wamepata 5, basi wewe umefaulu kama kipimo cha ufaulu ni 50. Hii ni sawa na kusema, ujihesabie haki kwa kutofanya sana uzinifu kama wanavyofanya jamii inayokuzunguka! Vipimo vya ukweli havilinganishwi na mtazamo wa jamii ‘’relative standards’’, hulinganishwa na vipimo vya haki ‘’absolute standards’’.

Kadri watu wanavyoshindana, ndivyo wanavyotazamia zaidi kuwa juu ya wenzao. Wengi wao sio watu wakutazama na kuona, bali hutazama na kulinganisha. Sio watu wa kusikiliza, bali husikia na kulinganisha. Idadi kubwa ya watu katika hatua hii ya tamaa, hushindwa kunufaika na ubora wa hali zao zisizolinganishwa.

Lengo La Lusifa

Lengo la Lusifa katika hatua hii, ni kuwatengenezea uhalisia feki wengi wa mateka wake. Mtu aliye na utajiri mkubwa sana lakini hana mamlaka huishi kama mtu asiye na kitu kabisa kwasababu tu ya kujilinganisha na aliyejuu kabisa zaidi yake. Vivyo hivyo mtu aliye na afya huishi kama vile asiye na afya kabisa kwa kujilinganisha na aliye na afya na mamlaka zaidi yake. Kiufupi lusifa analenga jamii isiyo na shukurani kwa hali walizonazo. Na matokeo yake ni kupata watu wasio na shukurani kabisa kwa hali walizonazo, ziwe za juu, ama za chini.

Wahanga Wa Tamaa Hatua Ya Pili

Viongozi wengi sana katika taasisi za umma, binafsi, na za kidini, wasomi wengi sana na vijana walio katika hatua za mafanikio, na wengineo wengi. Hawa wote hutekwa na lusifa kirahisi sana kutamani kuwa juu ya wengine. Na ilihali wakipambana sana kuwa juu ya wengine, hujikuta wakiingia katika wimbi la uraibu wa kutamani tamaa ya lusifa ya kuwa juu, na hapo ndipo msingi wa matatizo mengine yote.

3. Tamaa Ya Kuishi Milele



Hii ni aina ya tatu ya tamaa, ni aina ya tamaa ambayo hulenga kiwango cha mwisho cha tamaa ya mwanadamu. Yaani, mwanadamu alianza kutamani kuwa na uhakika wa Maisha, kisha akatamani kuwa na heshima na sifa juu ya wenzake, na sasa, mwanadamu huyu anatamani kuendeleza hali yake hii ya tamaa ya kuwa juu ya wenzake milele.

Na hapa ndipo utakuta wafalme wakijiita Mungu, hapa utakuta waheshimiwa wakubwa wakitaka upendeleo wa huduma bora zaidi za afya. Hapa ndipo utakuta matajiri wakubwa zaidi wakitaka kuwekeza katika miradi, au sayansi zitakazo wawezesha kuishi milele. Hali ya kuishi milele ni tamaa ya hatua ya mwisho ya tamaa, hali yoyote ile ya umilele, ni ya Mungu tu.

Viongozi wengi wakubwa hutamani uhakika wa ulinzi toka kwa idadi kubwa ya walinzi wenye taaluma kubwa kabisa.  Siyo kana kama huwa hatarini sana katika nafasi zao, ila ni kuwa huitaji usalama sana kutokana na nafasi zao. Wapo viongozi wengi wakubwa walioamua kuishi Maisha ya kawaida sana, hasa baada ya kuziona nafasi zao ni za kawaida sana. Na mara nyingi viongozi hawa huwa wachache sana kwa idadi, na huwa na Maisha ya kutojiinua kwa nafasi zao, kama wastani wa viongozi wengi.

Maana Ya Jaribu la pili la Yesu

Biblia inaandika, ‘’Kisha ibilisi akamchukua mpaka mji mtakatifu, akamweka juu ya kinara cha hekalu, akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu jitupe chini; kwa maana imeandikwa, Atakuagizia malaika zake; Na mikononi mwao watakuchukua; Usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe.

Jaribu hili linafanania kabisa hoja ya hatua ya tatu ya tamaa, ijapokuwa ni jaribu la pili. Jaribu hili linaonyesha ni kwa namna gani Binadamu huwa tunajaribiwa kwa tamaa ya kuwa na uangalizi wa Kiungu katika Maisha yetu ‘’divine intervention’’, hii ni kama namna ya kutamani kuwa na muunganiko na uwezo wa kiroho, uhakika wa asilimia 100%. Kiufupi tunarejea palepale katika kutamani kuishi milele.

Watu kadhaa hutamani hata kuambiwa kuwa wataenda sehemu Fulani baada ya Kufa. Lusifa anajua Kiburi cha mwanadamu yeyote yule huisha anapoeleka katika kufa. Na hutamani sana kumhakikishia kuwa hatakufa, aidha atabadilika kuwa kiumbe mwingine, au ataenda sehemu bora zaidi.

Watu Hutamani Kuwa kama Mungu

Katika hatua hii ya tamaa, ambayo inafungamana sana na hatua ya pili, iliyo katika jaribu la tatu. Watu wengi sana hutamani na kujaribu Kutenda kama Mungu. Watu hujiona wakiwa na uwezo wa kubadili majira na nyakati. Hujiona wakiwa na uwezo wa kuathiri Maisha ya viumbe wenzao. Hujiona wakiwa na uwezo wa kufanya lolote lile. Kiburi hiki huwasukuma sana kujiona kana kama wao si watu wa kawaida.

Hatua za wengi wa watu katika tamaa kiwango cha mwisho, huelekea kutawala kabisa wenzao. Wengi wao hutumia au hata kutengeneza dhiki nyingi sana kwa wanaowazunguka, na kutengeneza namna za suluhisho ambazo zitawafanya wanaowazunguka kuendelea kuwasujudia, na wao wakijilimbikizia nguvu juu yao.

Hutumia Sana Utajiri kama Silaha

Mara nyingi watu katika hatua ya mwisho ya tamaa. Hujikuta sana wakiegemea katika matumizi ya mali zao kutumia vikundi vya watu wa usalama kupambana na maadui zao. Kwao binadamu wa usalama huwa kama Malaika. Mara nyingi watu hawa huwachukia sana maadui zao, kwa kuwa wao huwa kama Mungu, na kisha maadui zao huwa kama wenye dhambi, na mshahara bora zaidi kwao huwa ni kifo.

Katika kizazi hiki watu hawa hutumia sana teknolojia za kisasa sana ili kuweza kujilinda, kwa kuwa na taarifa za kila kinachoendelea duniani kote. Watu hawa hutumia sana teknolojia katika namna mbili za kiuungu wao, yaani, kujilinda, na kujitukuza.

Sababu za Kupenda kuwa kama Mungu

Kusujudiwa huchochea kiini cha tamaa ya binadamu mpaka mwisho. Chuki zote, wivu wote, fitina zote, hasira zote, kiini chake ni kutamani kusujudiwa. Yaani, kuwa bora kuliko wote. Kama kuna mtu unamchukia mpaka mwisho, akija kukusujudia, maana yake yupo mbele zako akiwa chini mpaka mwisho, tayari kwa lolote utakalo. Ubongo wa binadamu hutamani sana hii hali ya kiungu, na wadhaifu wote huiota kama alivyo Lusifa mwenyewe aliyetamani kusujudiwa mpaka na Mungu wake.

Mungu pekee ndiye anaweza kufanya lolote, mwanadamu mpumbavu hutamani kuwa kama Mungu, kwa kiburi cha utajiri hujidanganya  kuwa anaweza Kutenda yote. Na hili hutokana na kuwa, mali nyingi huathiri afya ya ubongo, maana utajiri uliokithiri ni matokeo ya ubinafsi. Watu wenye akili nyingi hujali sana jamii zao, na hapo ndipo ulipo msingi wa ugunduzi na maarifa. Jamii yangu inateseka sana, na mimi kama nina akili, nitazitumia kuwasaidia, matajiri wengi huona dhiki za watu kama fursa, na kuzitumia kuwa juu yao, watu wa mtindo huu kamwe hawawezi kuwa na akili bora kabisa.

                           MATAWI YA TAMAA KISAYANSI

Yafuatayo ni matawi ya tamaa ambayo watu wengi sana hushikwa nayo kwa kuwa hushindwa kuelewa tamaa kiundani kabisa. Sehemu hii nitaelezea kiufupi msingi wa ubongo katika kuangukia katika mitego hii ya tamaa.

IBADA YA SANAMU & UCHAWI ‘’idolatry & witchcraft’’

Sitaelezea sana sehemu hii, kwa kuwa nimeandika kitabu kinachohusu sayansi ya ubongo inavyohusiana na mazingaombwe, uchawi, na miujiza. Katika kitabu cha Q6 msomaji atajifunza sehemu za msingi za ubongo katika sura mbili za kwanza, kabla ya kuelewa nini hutokea katika ‘’magic’’.

Kwanini ibada ya sanamu & uchawi na tamaa?

Kwasababu mitindo hii yote huusiana na kutumia na kuchochea sana sehemu za hisia, na sehemu za taswira ‘’imaginations’’, kupitia mfumo wa ubongo wa ‘’Default mode network’’, kadri mtu anavyojifunza uchawi, au anavyofanya ibada za sanamu, anajifunza kuvutia taswira kitu kilichombele yake, huku akielekea katika kuunda uhalisia tofauti na uliombele yake. Yaani, mtu anaona sanamu ya ng’ombe, ila anavuta taswira ya kutazamia mungu wake, hivyo hivyo kwa aina zote za wachawi, aidha kwa wale wa ‘’spell’’, ambao hunenea kitu huku akitegemea kutengeneza uhalisia wa kweli, wachawi hufundishwa kuvutia vitu taswira, hii huitwa ‘’visualization’’, na waabudu sanamu huingia katika kundi la wachawi la wasiotumia maneno, ‘’non-verbal rites’’, hawa hutumia sana ‘’Alama’’ au ‘’symbolism’’, nao hufanya pia ‘’meditation’’, hizi zote kwa Pamoja hukinzana na sehemu za ubongo zinazohusiana na uhalisia wa taarifa zilizopo mbele.

Madhara yake ni kuwa, mtu huingia katika uhalisia feki wa taarifa, kwa kuwa ubongo wake sasa kama ambavyo huonekana kwa namna unavyoathiri sehemu zake za ubongo zinazohusiana na utambuzi wa taarifa halisi ‘’parietal connectivity’’, huanza kupata taswira toka vyanzo visivyo na uhalisia. Kitaalamu ni mithili ya ‘’hallucinations’’, lakini kiuhalisia ni roho za kipepo ndizo huwa zikiwakamata watu hawa, na kuwaunganisha katika ulimwengu ambao wao huuona wa kiroho, kiufupi haya yote ni matatizo ya kiakili.

Tamaa imeingiaje?

Wengi wa wachawi hutamani sana kufikia hali za juu sana kihali zao za kiroho, hata kimwili. Wengi wao hupenda ulinzi na heshima. Wengi wao hutamani uwezo wa kuwadhuru maadui zao. Wengi wao hawapendi wawepo wenye mafanikio kuwazidi, au wenye kuwapinga. Waabudu sanamu pia hutamani sana ukaribu wao na miungu yao kiasi cha kutaka muitikio wa moja kwa moja kwa kuwa karibu zaidi na miungu yao. Na haya yote yamejengwa katika misingi ya tamaa, hata kumuasi Mungu wa kweli.

UADUI NA UGOMVI ‘’hatred & variance’’

Kwa utafiti mdogo sana unaoweza kuufanya, utagundua wengi wa watu hawagombani kutokana na kuwa hawawezi kukaa Pamoja na kutatua tofauti zao. Maana panapotokea mgogoro wowote ule, huwa kuna pande mbili ambazo watu hupishana, lakini ukweli ni kuwa, hakujawahi kuwa na kweli mbili. Na ukweli haujawahi jificha, kama watu wataamua kukaa Pamoja na kujadili pande zote kiundani kabisa, ukweli huonekana na watu hufanya maamuzi yaliyo sahihi.

Kwanini sasa Ugomvi na uadui?

Mara nyingi mmoja au wote huwa na tamaa. Marazote mmoja kwa tamaa zake za kutamani kuwa na mamlaka juu ya jambo linalogombaniwa, hupuuzia kabisa ukweli kuhusu upande wa pili. Uadui ni hisia za ndani za chuki. Lakini Ugomvi huwa ni matokeo yanayoonekana ya uadui.

Watu hugombana kwa kuwa mwenye ukweli huamua kuushikilia, na asiye na ukweli hutaka kutimiza matakwa yake. Ili hali wakigombana, wote sasa huwa wapumbavu. Maana baada tu ya uadui kuanza kama ugomvi, sehemu za hisia za wote wapinzani huwaka mpaka juu, na kama ilivyo kawaida hisia zinapoinuka, basi sehemu za akili za ubongo hushuka mpaka mwisho. Na ndiyo maana wenye busara huwa na uvumilivu sana kuzuia hisia kuwa na nguvu juu yao, hata wakashindwa kutawala misuli ya mikono, miguu, na midomo yao.

Popote pale panaposhamiri hisia za uadui, na kuibuka migogoro. Tamaa huwa zimejaa. Kadri unavyopanda ngazi za kimamlaka, ndivyo uadui na ugomvi huongezeka zaidi. Mpaka sasa msomaji anaweza kuelewa kwanini? ni kwasababu tamaa huongezeka toka hatua ya kwanza, mpaka hatua ya pili na tatu.

WIVU    NA HUSUDA ‘’emulations & envy’’



Kwanza wivu kwa kuutafsiri tu, ni tamaa ya kuzidi wengine, au tamaa ya kuwa bora zaidi. Wivu huwa ndani ya mtu ukiwa haujioneshi, lakini inapoonekana mazingira ya kuwa kuna aliye juu zaidi, wivu hujidhihirisha kwa hali ya kutotulia kiakili, au kuumia, au kutaka ashuke mpaka chini.

Husuda ni sawa na wivu?

Husuda huwa ni namna ya wivu ambayo tofauti yake na wivu moja kwa moja, ni kuwa Husuda hulenga zaidi hisia za chuki kwa kuona mafanikio ya wengine. husuda huwa hailengi mwenye wivu kutamani yeye kuwa juu. Mwenye husuda huumia kwa mafanikio ya wengine, lakini haleengi hata yeye kuwa juu.

Sayansi ya wivu

ubongo hulenga kumfanya mwenye wivu awe juu. hivyo kwanza, huchochea hali ya kutotulia ya kiakili kutokana na hisia za ubongo za ‘’sympathetic nervous system’’. ambazo huambatana na stress, kwa lengo la kumchochea mwenye wivu aongeze bidii, ili aweze kuwa juu. Hapa ndipo utakuta mwenye wivu akipambana sana ili kurejea kwenye hali yake ya awali ya kuwa juu.

Pili, mwenye wivu huwa na kiwango kikubwa sana cha homoni za stress, na hata homoni za dopamine, ambapo hizi na saketi zingine nyingi za ubongo huelekezwa katika kumfuatilia mpinzani wake, kwa lengo la kumuangusha, ila ubongo wake uweze kuzalisha homoni za serotonins, na endorphins nyingi, uweze kuburudika sasa. Hapa ndipo mwenye wivu huchanganyikiwa sana kisaikolojia, maana huteswa na kumbukumbu za mpinzani wake aliye juu, huteswa na mafanikio ya wenzake, na njia pekee ya kukabiliana na hali hii ya mateso ya kisaikolojia, huwa ni kubuni mbinu za kujituliza. Na hizi huwa ni kumfelisha mpinzani wake pale anapoweza, pili huwa ni kumchafua mpinzani wake pale anaposhindwa, na mwisho, huwa ni kutomfatilia mpinzani wake pale anapoona hakuna matokeo.

Je Wivu ni Hatari?

Kwa wenye wivu huwa ni hatari sana, maana idadi kubwa sana ya wenye wivu, huwa na tamaa, na tamaa huwafanya kuwa makini sana na wenye wivu wenzao. Bila takwimu unaweza gundua wenye wivu wengi huwa makini zaidi na wenye wivu wenzao. Hatari kubwa zaidi ya wivu ni kwa mwenye wivu, maana hushindwa kunufaika kwa Habari njema anazopatiwa, au watu wakubwa anaokutana nao. Kipindi Yesu anazaliwa, badala ya Herode kunufaika kwa Habari njema za ujio wa Kristo, anapata wivu wa kutaka kumuua, kwa kuhisi atachukua sifa au nafasi yake, na madhara yake akafeli yote.

HASIRA ‘’wrath’’

Hasira yenye matokeo makubwa sana kisaikolojia, hutumia neno hilo ‘’wrath’’. Mara nyingi watu walio na afya ya kiakili, huwa na msukumo wastani wa hasira, hii ni kwa kuwa, kama zilivyo hisia zingine, zinapovuka uwezo wa kujitawala, huchochea udhaifu. Hasira ni hisia za kukerwa kutokana na matokeo ambayo yanaonekana kuwa na madhara ya kimwili, au kisaikolojia. Mfano, kuvunjiwa heshima, kuumizwa mwilini, n.k.

Sehemu hii hasira haipo katika mantiki ya hisia zinazotokana na mifano hiyo juu, maana hasira ni muitikio wa asili wa mwili wa kujilinda. Hakuna asiye na hasira pale anapofanyiwa vitu hatarishi kwa mwili wake na akili yake. Mwili lazima utazalisha homoni kama adrenaline, cortisol, glutamate, noradrenaline, n.k. hizi na neva nyingi za fahamu huchochewa kusukuma muitiko wa haraka wa mwili wa kujilinda, ikiwemo kutumia nguvu za mwili kwa haraka na ustadi ili kujilinda, kwa kupambana, au kujiepusha.

Hasira kama tamaa?

Watu wenye hasira kupindukia, wote huwa na mfanano mmoja. Wote hutamani kuogopwa, kuheshimiwa kupindukia, kuwa na urahisi wa kulazimisha matakwa yao, na wengine hutaka hata kuabudiwa. Hasira za watu hawa huwa ni matokeo ya kisaikolojia, aidha kwa kujitengenezea, au kwa kutengenezewa, kama ambavyo huwa kwa wagonjwa wa ‘’post-traumatic stress disorder’’, yaani, watu ambao waliwahi kutendewa jambo ambalo liliwaumiza sana. Kiufupi lazima watu watambue, hali hii ya hasira ni hali ya tamaa ya kufikia hali ya amani ya kimwili, lakini kwa kupitia kuwafanya wengine wadhaifu, hii haina tofauti sana na zilivyo tamaa nyingine kama za wivu, na uchawi.

FITINA, FARAKA & UZUSHI ‘’strife, sedition & heresies’’



Fitina

Sifa kubwa ya mtu mwenye fitina, huwa haisi kama anaweza kukubaliana na hali Fulani. fitina ni hisia zinazosukuma hali ya upinzani, ndani ya kikundi, hata wakati mwingine ndani ya mtu binafsi. Fitina ni tawi la tamaa ambalo wakati wowote hujidhihirisha kwa kuleta matokeo hasi kwa nje. Mwenye wivu hutofautiana kidogo sana na mwenye fitina, wote huchukia hali zilizopo juu yao, tofauti yao ni kuwa, mwenye fitina huwa na hisia za ukinzani zinazotokana na sababu nyingi, wakati mwingine, mitazamo yake binafsi. Mfano, mwenye fitina anaweza kuwa marazote tu akimchukia mtu Fulani, kwa kuhisi tu mtu huyo anasifa Fulani mbaya.

Kwanini fitina ni tamaa?

Marazote wenye fitina huwa hawawezi kukinzana na hali yao ya chuki dhidi ya wapinzani wao, kwa kuwa sababu zao huwa hazitokani na sababu za nje ambazo wangeweza kuzitatua, huwa zinatokana na sababu zao za ndani za tamaa. Sababu za kutamani wapinzani wao wadhalilike, au wafeli, ili wao waweze kuwa na nafasi, au amani.

Faraka

ni hali ya kuibua hisia za ukaidi dhidi ya mamlaka, au mfumo Fulani uliopo. Mfano, penginepo mwenye fitina angeweza kuibua hisia za kuwa, mwandishi wa kitabu hiki ni mkaidi, na anachochea chuki dhidi ya mifumo yenye nguvu. lakini ili maana ikamilike ya fitina, lazima tuangalie dhumuni la hoja ya ukaidi. Mwandishi wa kitabu hiki angeonekana akiwa na lengo la Upendo, na kuikoa jamii kwa upendo, na amani, bila hasira, uadui na ugomvi. Lakini mwenye fitina huwa na dhumuni la Tamaa, la kuchafua hali iliyopo, ili aweze kupata nafasi ya kuwa juu ya wengine.

Wenye fitina wengi sana utawagundua kwa namna huwa hawana taarifa za kutosha kuhusiana na hoja wanazozichafua, wengi wao huwa hawana kiasi, waropokaji, hii yote ni kwa kuwa, hisia za fitina zinatokana na matatizo ya kisaikolojia. Na fitina huambatana moja kwa moja na hisia za uadui, na hisia za ugomvi.

Uzushi

Uzushi unatokana na hali za kuzusha. Kuzusha kunamaanisha kuibua. Kuibua kunamaanisha kutoa toka sahihi, na kupindisha. Kwa kiingereza unaweza tumia neno ‘’deviate’’. Wazushi ni watu ambao huibua hoja zao toka kwenye ukweli, na kuzipaka rangi na kuzizusha. Wapo ambao hufanya makusudi wakijua, lakini wapo ambao hufanya wakiamini wamegundua udhaifu uliokwepo.

Kwanini uzushi ni tamaa?

Marazote wazushi hutamani kupata heshima, na sifa, toka kwa watu, kama wao ni watu makini kuweza kugundua udhaifu uliopo. Wazushi huwa na tamaa ya kuwa nje na mifumo yao, ili kuonekana wao wapo makini zaidi, au wenda, wao wana uwezo mkubwa zaidi.

Wazushi wote hawana kiasi, wazushi wote hutumika sana kuchafua mamlaka na mifumo safi kabisa. Wazushi wengi huwa wasaliti, na wengi wao huwa ni wagonjwa wa kisaikolojia.

Saikolojia ya fitina, faraka & uzushi

Wote wenye sifa kati ya hizo juu tatu, huwa na tatizo moja kubwa. Huwa hawana uwezo wa Kuzingatia na kutawala hisia zao. Wengi wao ni wadhaifu wasio na uhuru wa kifikra ‘’open mindedness’’. Huweza kupata ukweli, lakini kwa kuogopa kubadilisha misimamo yao kwa kufatilia kwa kina, hupuuzia. Wengine hawana hata uwezo wa kufatilia mambo kwa umakini sana hata wakayaelewa, na hujikuta wakizusha tu.

Wenye fitina wengi huwa na namna ya tofauti kidogo ya wivu, na hushindwa kutatua changamoto zao kwa hisia za uadui, na huishi Maisha feki ya chuki kwa majirani wao, huku wakiwatamania mabaya. Haya yote ni makundi ya tamaa.

ULEVI ‘’drunkenness’’

Unaweza soma kitabu cha Q4 kuelewa kiundani madhara ya afya ya ulevi, na madhara ya pombe kuanzia tumboni, katika ini, mpaka katika ubongo. lakini unapozungumzia ulevi, unazungumzia madhara ya kupoozesha, au kulewa, au kuzubaisha akili, kwa kutumia vileo, ambapo hasa zaidi ni pombe. Zipo namna nyingi za vitu vya kulevya, kuna madawa ya kulevya, kuna bangi, shisha, n.k.

Kwanini ulevi ni tamaa?

Tofauti ya mlevi na mchawi, ni kuwa mchawi akishalewa anazungumza na mapepo, lakini mlevi akilewa anarudi nyumbani. Wote kwa Pamoja wanakimbia uhalisia wa Maisha yao ya kawaida. Mlevi anaamini akishakunywa pombe, ataingia katika hali ya utulivi wa kiakili, na katika namna mbalimbali walevi hujikuta wakishakuwa waraibu, hii ni kutokana na matatizo ya ubongo katika sensa, au ‘’receptors’’ za ubongo, kama ‘’GABA, na Glutamate’’, na hata ‘’Dopamine’’, unaweza soma Q4 kuelewa kiundani uraibu wa pombe ‘’withdrawal syndrome’’.

Ulevi ni tamaa ya kuwa huru toka katika uhalisia wa Maisha ya kawaida. Watu wengi ambao huchochea ulevi, huchochea hali za kiburi, za kutowaza, za kutojali. Wasomi wengi hawajui madhara ya pombe huanza hata kabla ya pombe, wengi huanza na kiburi na kujipa hisia za kutojali hata kabla ya kunywa, na hapo ndipo unapoweza kuthibitisha hisia za tamaa, za kutaka kuwa nje ya mfumo wa akili za wengine, ambapo kwa mlevi ni wote mnaomtaka asinywe.

Hali ipo hivyo hivyo kwa wavuta sigara, bangi, shisha, madawa ya kulevya, n.k. kiufupi matatizo huwa makubwa sana kabla ya wengi wao kuanza, lakini short cut ya kufikia hali bora kabisa ya kiakili kupitia ulevi ndiyo huwaathiri wengi.

ULAFI ‘’revellings’’

Ulafi ni hali ya kushindwa kujitawala katika hamu ya chakula. Ulafi ni tamaa ya kula mpaka mwisho. Marazote ili mtu awe mlafi, lazima mfumo wake wa ubongo wa hamu za kula, na kuridhika kwa chakula uathiriwe ‘’disruption in orexigenic pathway’’. Na vyakula ambavyo vinaweza kumuathiri mtu hata akaingia katika hali hii ya ulafi nimevielezea vizuri sana katika Q4.

Kwa ufupi sana, Ulafi hutengenezwa zaidi ya kutokea kwa asili. Watu wengi walafi hufikia hatua hiyo kwa kula sana vyakula vyenye msisimko mkubwa sana wa Ladha, kuliko wastani wa asili. Madhara yake mfumo wa homoni wa hamu za kula huathirika. Mfano mwepesi ambao huwa napenda kuutumia ni kuwa, kijiko kimoja cha sukari ni wastani sawa na mtu anayekula mita moja ya muwa, lakini mtu mmoja anayekunywa soda moja tu, huwa na wastani unaokaribia wa vijiko kumi vya sukari. Hiyo ni sawa na kusema mtu anayekunywa chupa moja ya soda ni sawa na mtu anayekula mita kumi za muwa, jambo ambalo linaonyesha ni triki tu ya ubongo iliyechezwa na wazalishaji wa bidhaa hizi.

Ulafi hukua kwa matumizi ya vyakula vyenye vichocheo vingi kupita wastani unaohitajika, mfano, sukari nyingi watu ambayo hutumia katika bidhaa za kisasa huwa kiundani haihitajiki mwilini, watu wengi hula nyama kwa kiasi ambacho kiundani hakihitajiki mwilini, mfano, kwa wiki nzima mtu mzima angehitaji nusu kilo tu ya nyama, na hapo bado takwimu huonyesha ni nyama ambayo angebidi kuipunguza zaidi. lakini watu hutumia maranyingi zaidi ya wastani. kiwango cha pombe ambacho mwili ungekivunja ni kidogo sana na uhalisia wa kiwango ambacho watu hutumia hata kulewa. Haya yote yanachochea kuwa, ulafi hutengenezwa sana kwa triki za kiakili, ambazo nilizielezea sana katika injili ya sayansi Q4, ikiwemo kucheza na uzalishaji wa homoni ya msisimko ya dopamine, na kuchochea tabia za ulafi.

Walafi wengi sana sio wakarimu, hawana kiasi, hiyo yote ni kutokana na tamaa zilizokithiri za vyakula, ambazo huwaathiri hata afya zao za kiakili.

UFISADI

Ufisadi ni neno linalomaanisha matumizi mabaya ya mali za umma kutokana na mamlaka. Ufisadi huwa na familia yake ya tabia, kama vile rushwa, wizi, n.k.  ufisadi moja kwa moja ni tamaa ambayo inatokana na kutamani zaidi ya mamlaka uliyopatiwa, na kibaya zaidi, mafisaidi wengi huwa ni wasiri sana wa wizi wao wa mali za umma.

Tofauti ya fisadi na mwizi, ni kuwa mwizi hutambulika na husukumwa na tamaa zinazotokana na kutokidhi hali yake, au hata tabia ya kutamani zaidi kwa njia ya kuiba. Lakini fisadi huwa ni mtu asiye mwaminifu kwa ndani, lakini kwa nje kuvaa huusika mwingine. Fisadi ni mnafiki kwa mamlaka anayoshikilia. Mara nyingi fisadi hupelekea madhara makubwa zaidi ya mwizi, kwa kuwa huwa na nafasi rahisi na endelevu zaidi ya kuiba, na hata kujilinda dhidi ya kugundulika. Watu hawa huwa wanatamaa sana, na huvikwa roho ya ubinafsi, na ukatili, na hata uuaji kwa wanaowagundua. Mungu huwachukia sana watu wenye tamaa hata wakafikia hatua hii.

 

UZINZI, UASHERATI& UCHAFU

‘’adultery, fornication, uncleanness, lasciviousness’’

Uzinzi ni tendo la ndoa kabla ya ndoa, kwa wasio wanandoa. Uasherati ni tendo la ndoa, kwa mwenye ndoa, na asiye na ndoa. Uchafu ni matendo yote yanayohusiana na kufanya mapenzi katika namna zisizo za kimaadili, au za kisasa zaidi kama utazamaji wa filamu za ngono, na kutumia vitu, au namna zisizo za asili katika kujiridhisha kimapenzi.

Lusifa na mapenzi

Lusifa anapenda sana kutumia tendo la ndoa ‘’sex’’ tangia zamani sana za kipagani. Lusifa hupenda sana hisia hizi za mapenzi kwa kuwa, huwafanya watendaji kuwa dhaifu sana kiakili. Hii ni kwasababu marazote mapenzi husisimua sana hisia kiasi cha kuzimisha kabisa sehemu za ubongo za kutafakari, na matokeo yake ni kuwa, watu wengi huwa hatarini sana kuvamiwa na roho chafu, au hata Kujawa na uraibu kwa kushindwa kujitawala kihisia, pale yanapofanyika kinyume na utaratibu wa kiasili.

Marazote jamii za kipagani, na taasisi za kiumizimu huusisha mionekano ya utupu, au hata matendo ya kiuzinzi. Lengo hasa huwa ni kudhoofisha kabisa uwezo wa kiutambuzi wa watu. Lusifa hasa katika mitindo ya kisasa amechochea zaidi uhuru wa tabia za uchafu wa kingono, wengi hawajui ni nini sababu ya msingi kabisa ya kuchochea mitindo hii  ya zinaa kupitia miziki, filamu, na mitandao ya kijamii. Malengo makuu ya lusifa ni kama yafuatayo:

Kama tulivyoangalia katika Q4, kadri watu wanavyoangalia taswira zozote zile, huwa wakijiunganisha nazo, hii tuliona kupitia uwepo wa seli za kuiga, yaani ‘’mirror neurons’’, katika maeneo ya juu ya ubongo kama ‘’premotor areas’’, maeneo haya huusiana na msisimko wa mwili moja kwa moja. Kadri watu wanavyotazama taswira za uchi, ndivyo wanavyoingia katika msisimko wa via vya uzazi, na kutamani zinaa moja kwa moja.

Hoja sio kutamani tu zinaa, hoja ni kuwa, kadri watu wanavyoingia katika hisia za mapenzi, au ngono katika mazingira yasiyo na utakatifu, huwa katika hatihati ya ubongo wao kuwa hatiani kuvamiwa na roho za uchafu. Wanasayansi baadhi hujifanya hawaamini roho hizi, lakini huamini Aliens, na wakati huohuo wengi wao huwa wanachama wasiri wa vyama vya kishetani. Wapo baadhi ni wahanga kabisa wa Imani za ushirikina, lakini kwa nje hujifanya hawaamini Imani za roho hizi, injili ya sayansi haina muda wa kuhangaika na wasomi wanafiki.

Tabia za Kujisugua ‘’masterbation’’, na Pornography

Hawa wote ni kielelezo cha ngazi ya juu kabisa ya tamaa. Yaani mtu anatamani kitu ambacho hakipo pale, na ubongo wake unatengeneza uhalisia wa kana kama yupo pale. Hakuna mwanamke aliyelala kwa ajli ya zinaa, lakini mtu kupitia network yake ya Ubongo, ya ‘’Default mode network’’ anamtengeneza binti kichwani, anampeleka katika sehemu yake ya ubongo wa mbele, anamuandaa, na sehemu yake ya hisia inasisimka kiasi cha kuchochea Ubongo sehemu ya Hypothalamus-tezi ya pituitary, mpaka via vya uzazi vinasisimka kwa ongezeko la mtiririko wa damu mithili ya mwanaume anayefanya zinaa halisi, mtu huyu mfumo wake wa PSNS ‘’parasympathetic nervous system’’ husisimka na kumfanya aendeleze mhemko wa via vyake kama mtu aliye kwenye zinaa kweli, katika Q4 nilielezea madhara wanayopata watu hawa kiafya, lakini katika sehemu hii nalenga kuonyesha namna watu hawa mfumo wao wa ubongo unavyoathiriwa, na kutengeneza gepu pana sana lililo wazi la roho chafu kuingia katika sehemu zao za ubongo wa mbele, na kuwatengenezea uhalisia na uraibu, na hata kuwatawala kabisa kifikra.

Tabia za Uchafu wa Kingono

Mara nyingi watu hawa huwa wamejawa na roho za ngono zilizovuka wastani wa kawaida. Kwanini? ni kwakuwa maranyingi watu wenye uchafu katika mitindo ya kingono, huwa tayari ni wahanga wa hatua za kwanza za ngono. Wengi wao kama nilivyoeleza katika kitabu cha ‘’Ubongo wa mtu mweusi’’ huwa hawasisimki tena na utendaji wa ngono katika mitindo ya kawaida. Wengi wao huwa hawana nguvu za kiume aidha, au huwa wahanga wa mitindo ya zinaa tangia udogoni, hivyo huwa wakitafuta namna za kujiridhisha zaidi, maana ubongo wao huwa na msisimko mdogo zaidi kwa njia za kawaida za tendo la ndoa.

Utazamaji wa filamu za kisasa zilizojaa picha, na mionekano ya kizinaa tangia umri mdogo, huathiri ukomaaji bora wa ubongo, na uwezo wa kuwa na kiasi katika kutawala mihemko ya kimwili. Wanaume ambao huwa na tabia za kishoga wengi wao huwa hawasisimki kabisa kwa tendo la ndoa la asili kati ya wanaume, na wanawake. Hakuna shoga anayeingiliwa kinyume na maumbile akawa sawa kiakili, lazima atakuwa alikuwa mwathirika wa PTSD awali, lakini baadaye akajifunza uwendawazimu. Ukirejea kitabu cha Q5 unaweza kuelewa kiundani kabisa hoja hii yenye misingi mipana katika fiziolojia ya ubongo.

SILAHA TEGEMEZI YA LUSIFA

Lusifa anapojua kuwa hana namna nyingine yoyote ile ya kuwashinda watu makini wa Mungu wenye maarifa. Hutumia njia za kuwatega kihisia kuwatega kwa tamaa za kimwili. Kiufupi hisia za mapenzi huwa hazihusishi uwezo wa kutafakari, na kama utaweza kuwafanya watu wasitafakari, hata wenye maarifa makubwa unaweza kuwateka katika gari la uharibifu.  Kwa wastani katika mitandao ya kijamii, huwa kuna picha za wanawake wanaojipost 3 mpaka 4 kwa1 ya wanaume. Hii ni kwa mitandao kama Tiktok, Instagram, na Facebook ikiwa kwa wastani mdogo kidogo.

Watu wengi hawajui kwanini picha nyingi zaidi huwa ni za kike, sababu ni kuwa, wanaume husisimka sana kwa kutazama, zaidi ya wanawake. Ambapo wanawake husisimka zaidi kwa mambo wanayoyasikia, na hii ndiyo sababu wanawake hushawishiwa sana na mienendo ya kijamii, kama nilivyoeleza katika Q5, hata sehemu za ubongo za wanawake za lugha zimeendelea zaidi ukilinganisha na kwa wanaume. Wanaume huathiriwa zaidi na mitandao ya kijamii kwa kuamshwa kitamaa za ngono, huku wanawake wakiathiriwa zaidi kwa mitandao ya kijamii, kwa kutamani  Maisha ya kifahari na kuwa na wafuasi wengi. Haya yote ni matokeo ya tamaa, na huchochea tamaa, na humtukuza lusifa.