Jipatie maarifa kutoka vitabu bora vilivyoandikwa na Dr Brighton shoo kuusu imani, sayansi, afya, teknolojia, asili, malezi, saikolojia na mazingira

LUSIFA DHIDI YA KAZI #4

LUSIFA DHIDI YA KAZI

Kama Nyoka

Lusifa kwa karne amekuwa akiwachochea watu Kwenda kinyume na malengo makubwa ya kazi, na mashine. Lusifa anajua amri ya Mungu inawataka watu kufanya kazi kwa siku sita, na siku ya saba kupumzika. Huwezi pumzika bila kufanya kazi, kazi imepewa kipaumbele kwa asilimia zaidi ya 85% katika maisha ya mwanadamu. Mwanadamu anapofanya kazi, ndivyo anavyozidi kuishi bora kiuchumi, na kiafya. Mwanadamu anapovunja tu sheria hii, huwa hatiani kwa kila aina ya matatizo.

Lusifa huwajia watu na triki ya kuwasaidia wapunguze kazi kama namna bora kabisa ya maisha. watu bila kujijua hukimbilia sana kazi rahisi, ambazo huwa zimerahisishwa na watu wachache sana waliofanya kazi ngumu sana. Kwa kupenda mitindo rahisi kimatumizi ya misuli, utokaji wa jasho, hatari za changamoto, watu huisi wanaweza kukimbia Laana ambayo Mungu aliitoa Edeni kwa wazazi wetu wa kwanza, lakini madhara yake hujikuta wakipatwa na matatizo makubwa zaidi hata ya Laana ile rahisi sana ya kutokwa na jasho, na kupambana na miiba, au kuzaa kwa uchungu.

Mashine zimetapakaa katika ulimwengu wa ubinadamu, lakini ajabu ni kuwa, mashine hizi nyingi hazitumiki kuwasaidia wanadamu wengi zaidi, bali kuwainua binadamu wachache sana. Teknolojia na taaluma kubwa za mashine zipo chini ya nchi kubwa sana zilizoendelea, ambapo huficha taaluma hizo na kuwafanya wengine kuwa wateja wa bidhaa zao, na kuchukua nafasi za vijana wao, viwanda vimesheni silaha za kuhatarisha maisha ya watu, idadi kubwa ya teknolojia zinawaondoa watu toka mazingira yao ya asili, na kuwaingiza katika mazingira mapya hata kifiziolojia. Watu wamekuwa sio wakufikiria tena nje na wanavyoviona, maana kazi wanazozishuhudia nyingi ni kazi za watu, zilizojaa siri nyingi na historia pana sana.

Kwa kawaida Ubongo huwa unakimbia matumizi ya kazi ‘’Procrastination’’, ili kutunza nishati yake. Na ndiyo maana mwili huwa unapenda kula na kulala au kubebwa, na haupendi kazi, kuoga na kufikiri. Mwili haupendi kazi, ila unaihitaji kazi ili uweze kuwa imara. Na sasa basi, Lusifa hutumia huu udhaifu kuwatriki watu wengi. watu wengi wangependa kazi za kukaa tu chini, au kutumia nguvu kidogo sana.

Matumizi ya Roboti ‘’Robotics’’, na Akili za kisasa ‘’Artificial intelligence’’, yamezidi kushamiri, watu wakiwa hawataki hata kufikiria. Wakiamini wanaweza kupata majibu ya matakwa ya akili zao kwa kuuliza tu. Lakini kila kilichomo katika mashine hizi, ni taarifa iliyokwisha kuwepo, mwanadamu anapaswa kusogea mbele kila wakati, ni lini mwanadamu huyu ataenda mbele kama kila anachotazamia ni kilichokwisha fanyika. Lusifa anatambua anapaswa kumrudisha mwanadamu kwa gharama yoyote ile, kurejea katika upumbavu wake wa awali. Wanafunzi hawajichoshi tena kusoma historia kama zamani, wengi wapo juujuu sana kimaarifa. Hata hawaelewi Mashine hizi zimetengenezwa kwa ajenda maalumu. Majibu mengi kutoka mashine hizi huwa na falsafa za ukana Mungu, na itikadi za ukoloni wa kiakili. Zimetengenezwa  kuchochea uabudu wa mifumo, serikali, na watu baadhi, kuliko maarifa ya kweli, na Mungu na watu wake.

Watu wa kawaida wengi huona Fahari sana kumiliki magari ya kifahari, ndege, silaha, mashine za kisasa na thamani, n.k. lakini wengi wao ni wapumbavu sana hata kushindwa kujua kuwa dhumuni la mashine hizo sio kubadilisha matumizi ya viungo kutoka kutumika, hata kutulia, bali ni kusaidia pale viungo vyao vinapokuwa vimefikia kikomo cha uwezo wa kutembea. Yaani, dhumuni la gari, ni kukusaidia utakapokuwa umeshatembea vyakutosha hata kushindwa kuendelea zaidi, lakini bado unahitaji kufika mbali zaidi. Gari lipo kukuwezesha kufika miguu yako itakaposhindwa, sio kutumika pale ambapo miguu ingepaswa kutumika. Lusifa amezidi kuathiri watu kwa kuwafanya kuhisi thamani za mashine zao, ni uwezo wao mkubwa wa kiuchumi wa kuweza kuzilimiliki, na sio dhumuni la kuwasaidia kufikia malengo yao. Na hapa ndipo utakuta mtu  mmoja akimiliki magari 100, huku majirani zake wakiwa hawana hata baiskeli. Huyu kwake magari, ni Fahari.  Matajiri wengi wamekuwa wakiishi maisha ya hovyo kabisa, wakiwa hawana amani kama walivyo tu watu wasio na uhakika wa kupata mlo hata mmoja kwa siku. Lusifa amewavisha mavazi ya heshima na utukufu kwa nje, lakini kwa ndani amewajaza maumivu, mateso na majuto.

Lusifa ameondoa ukweli juu ya dhumuni la kazi. Kazi ipo kwa lengo la Ibada, kila mtu anapofanya kazi, anarejea kazi ya siku sita za Mungu za uumbaji. Kazi inaleta Faraja na furaha, mwili huzalisha Dopamine kila kazi inapokamilika. Kazi ipo kujenga afya, mwili huvunja kila mafuta hatarishi, maji na damu huimarisha mzunguko wake kwa kila kazi inapofanyika, kazi hujenga familia na ushirikiano kwa asili yake ya ushirikiano. Kazi ni msingi wa ukuaji, mwanadamu hufunguka kimawazo na kiuchumi kila anapofanya kazi. Lakini Lusifa ameifanya kazi kuonekana ni mateso, ambayo watu wenye mafanikio huifanya kuwa ndogo hata kutoifanya kabisa. Lusifa ametengeneza kazi kuonekana ni uwanja wa Vita na mashindano. Watu wanafanya kazi ili kuonekana, au kuwa juu zaidi ya wenzao. Kazi imeonekana ipo kwa ajili ya kuishi, na sio kuishi kwa ajili ya kazi. Mwanadamu hakuumbwa na kazi, ila mwanadamu ndiye aliyeumba kazi zake baada ya kuishi. Leo hii kuna kazi nyingi ambazo zamani hazikuwepo, hii ni kwa kuwa kama mwanadamu aishivyo, ndivyo hutengeneza kazi mpya kila siku.

Kama Joka

Lusifa kama joka huwamaliza wote aliowafanya kuichukia kazi. Lusifa huwafanya wanaume kuwa kama wanawake, na wanawake kama wanaume kupitia kazi. Mwanaume tangia akiwa mdogo sio kiumbe wa kukaa chini, na ndiyo maana hana uwezo wa kuvumilia kukaa kwa muda mrefu. Kitaalamu mwanaume ana ‘’BMR’’ kubwa, akiwa na misuli mikubwa, na mafuta kidogo. Lusifa amewaweka wanaume wenye sifa nzuri za kiume katika kiti kwa miezi mpaka miaka, sasa wamekuwa na mafuta mengi tumboni, amewafanya kuwa na pumzi ndogo sana za kustahimili nyakati za ukakamavu, amewafanya kukesha usiku na mianga ya taa za umeme na kuwashushia homoni za kiume kama ‘’testosterone’’, sasa wanaume sio wenye maamuzi magumu tena kama zamani.

linganisha mwanaume wa picha ya awali, na wanaume wa picha ya chini.

unaweza tabiri hali za uanaume baina ya tabia zote katika picha hizo.

Maelfu ya watu wanashida zinazotokana na mitindo yao ya kazi. Wapo ambao maisha yao yameshamiri katika mitambo inayowafanya kufanya kazi ambazo zinatumia sana aina moja tu ya misuli, hata kudhoofisha sehemu zingine za miili yao. Wapo wafanyakazi ambao hawana kazi kabisa za misuli yao kama ambavyo wangepaswa, na ugumu wa ratiba zao, wengi wa watu hawa hata muda wa mazoezi huwa hawapati. Lusifa amewafanya watu kuwa na stress nyingi makazini mwao, wengi wao makazini hutumia vyakula dhaifu kabisa kwa afya zao. Kazi nyingi sana zimezidi kuwa za kusaidia utendaji kazi wa mashirika, kuliko kazi ambazo zina maslahi ya moja kwa moja kwa watu. Lusifa anajua hii ni namna bora zaidi ya kuwafanya wafanyakazi hawa kuwa watumwa wa mashirika yake, na serikali.

Lusifa anajua kadri anavyowakusanya watu wengi katika mitindo yake ya kazi, sehemu kubwa sana ya watu watakosa kazi. Hii imepelekea dunia nzima kuwa na kilio cha upungufu wa kazi, lakini wakiisema kazi kama ajira. Lusifa alishajua tangia awali, kama watu hawatajua msingi wa kazi tangia awali, wengi hawatajua lengo la kazi lilikuwa ni kushea nguvu na maarifa, na sio kujikusanyia. Kama kila mtu atakuwa akijikusanyia, baada ya muda lazima watu wengi watakosa. Hebu chukulia mfano huu, kama Nchi nzima inamzunguko wa kiasi ‘’XXX/=Tsh’’ kwa watu wote, na katika mzunguko huu, watu kadhaa wakawa na nguvu ya kujikusanyia zaidi ya wengine, nini kitatokea baada ya muda? Bila shaka haiihitaji hisabati kujua baada ya muda, wengi wa watu watabakiwa na kiwango kidogo sana cha thamani, na kadri siku zinavyoenda, ndivyo hata duniani tunavyozidi kushuhudia familia chache tu zikizidi kuwa na Nguvu zaidi kiuchumi, na tena, zikiwa na nguvu hata kisiasa. Hili lilikuwa lengo la Lusifa la kuja kuua kabisa mfumo wa kazi kwa binadamu.

Malengo ya Lusifa yalikuwa ni kuhakikisha anafanya watu wengi zaidi katika jamii kushindwa kufanya kazi. Maana hawana pakufanyia kazi, hali za maisha na hewa zinazidi kuwa ngumu, wengi  hawana nafasi katika mashirika na serikali. Lusifa anazidi kuchochea hisia za ukaidi, ukatili, hasira, na hata unyang’anyi kwa vijana hawa waliochini, Lusifa anajua wakati mbele kidogo atainua Chuki kubwa ndani yao, na atatumia ghadhabu yao dhidi ya mifumo iliyojuu yao kutengeneza migogoro mikubwa ya amani, na amani haitakwepo tena mpaka Yesu atakaporudi.

Mafanikio ya Lusifa ni makubwa sana katika kazi. Asilimia kubwa ya vijana waliokuwa wanahitaji kazi, sasa hawana kazi. Idadi kubwa ya mazingira ambayo watu hawa wangeweza kutengeneza kazi, hawawezi tena kuwepo, wala kuyamudu. Maana Lusifa ameshachochea uharibifu mkubwa kabisa wa mazingira kama tutakavyoona mbeleni kidogo.